Mwanamke aliyepona saratani baada ya kuondolewa viungo vinane

Chanzo cha picha, Faye Louise
Mwanamke mmoja wa Uingereza ambaye alilazimika kuondolewa viungo vyake vinane kutokana na saratani ambayo ni nadra sasa amepona na kurejea kazini.
Hii ni simulizi ya Faye Lewis kutoka Horsham, West Sussex.
Mnamo 2023, madaktari waligundua uvimbe kwenye utumbo. Faye alifikiri atakufa na hata alipanga mazishi yake mwenyewe.
Hata hivyo, upasuaji mkubwa uliokoa maisha yake na kumwokoa kutokana na saratani.
Faye, ambaye anafanya kazi kama msafirishaji katika Uwanja wa Ndege wa Gatwick, sasa amerejea kazini mwake.
Faye alisema kuwa kupona saratani ilikuwa "zawadi nzuri ya Krismasi" kwake. Faye anasema mwaka jana hakuwahi kufikiria kuwa atafanya kazi kwa wakati huu.
"Kazi yangu inahitaji bidii ya mwili. Lakini napenda usafiri wa anga. Nina furaha sana kurejea kazini," aliiambia BBC Radio Sussex.

Chanzo cha picha, Cancer Research UK
Hedhi
Faye ni mwanamitindo wa zamani ambaye alihisi maumivu tumboni mwaka wa 2023. Mwanzoni, alifikiri ni kutokana na kipindi chake.
Uchunguzi wa ultrasound ulionyesha uvimbe kwenye ovari yake. Faye alifanyiwa upasuaji.
Hata hivyo, baadaye iligunduliwa kwamba alikuwa na saratani. Madaktari walimgundua na uvimbe adimu unaoitwa pseudomyxoma peritonei. Hii husababisha dutu inayofanana na jeli kujiunda kwenye tumbo. Uvimbe huo ulipasuka na kueneza seli za saratani katika mwili wake wote. Faye alilazimika kufanyiwa upasuaji. Viungo vyake vinane vilitolewa.
Upasuaji huo uliondoa kiungo kinachochuja damu (Spleen), kibofu nyongo, ovari, uterasi, mirija ya uzazi, kiambatisho, kitovu cha tumbo, sehemu ya ini, (mfuko kwenye utumbo) inayounganisha tumbo na viungo vingine.

Chanzo cha picha, Cancer Research UK
Faye lazima apimwe uchunguzi kila mwaka mnamo Novemba ili kufuatilia afya yake.
"Kusubiri matokeo siku zote ni msongo wa mawazo, kutaathiri sherehe zangu za Krismasi. Lakini ninajaribu kuwa imara na kusonga mbele," Faye alisema.
"Siku chache zimekuwa ngumu, lakini kila kitu kiko sawa," alisema.
Faye amerejea kazini na pia amekuwa akichangisha pesa kwa ajili ya Utafiti wa Saratani Uingereza. Mojawapo ya hafla zake za kuchangisha pesa ilikuwa kupaka rangi ya chungwa kwenye baa ya Red Lion huko Slinfold. Pia alikamilisha 'Mbio za Maisha' katika Stanmer Park nchini Uingereza kwa ajili ya kutoa misaada.