Waridi wa BBC: ''Nilimpata mume wangu kupitia mtandao wa kijamii''

Chanzo cha picha, Alice Njeri
- Author, Anne Ngugi
- Nafasi, BBC Swahili
Alice Njeri au kwa jina la lengine akifahamika kama Jeje Ndung’u , ni mwanamke kutoka Kenya anayeishi jimbo la Washington nchini Marekani. Miaka nane iliyopita alifunga ndoa na barafu wake wa moyo , mume wake. Safari ya kupata mpenzi anasema ilimtosa hadi mitandao ya kijamii alikofanikiwa baada ya misukosuko katika ulimwengu wa mahaba .
“Niliyona miaka yangu ilikuwa imesonga , na kutokana na changamoto za aina ya ajira niliyokuwa nayo , nilijipata nikiwa sina nafasi ya kujenga urafiki na mwanamume kikawaida yaani watu wengi wanavyokutana na kupendana “anasema Jeje

Chanzo cha picha, Alice Njeri
Jaribio la kwanza mtandaoni
Kwa hio mama huyu aliamua kutumia teknolojia kama jibu la kutafuta mume , anasema kwamba licha ya mengi aliyokuwa ameyasikia kuhusu utapeli wa hali ya juu, uongo kuweko katika baadhi ya mitandao ya mahaba hakukata tamaa. Kwa hio aliunda utaratibu wa kujitambulisha kwa wapenzi kwa mfano alichokuwa anatafuta ni ndoa na mtu mwenye ndoto ya kuanza familia ila mara ya kwanza alipoanza anahisi alichezewa shere, alikutana na watu tofauti ikiwemo kisa hiki.
“Mara ya kwanza nilikutana na mwanaume mmoja na tukaanza mawasiliano, alikuwa jimbo tofauti na nilipokuwa naishi ,Kwa hio tuliwasiliana na hatimaye tukatenga siku ya kukutana,niliabiri ndege hadi jimbo la Michigan kutoka jimbo nililokuwa naishi la Seattle amini usiamini hakutokea na wala hakuwasiliana nami, nilimsubiri hadi siku inaisha”anakumbuka Jeje

Chanzo cha picha, Alice Njeri
Mwanamke huyu anasema mara ya kwanza ya kujaribu kujenga urafiki wa mapenzi mitandaoni hali haikuwa Sawa , alimsubiri rafiki wake wa kiume asionekane.
Kwa siku tatu ilibidi akae jimboni humo hadi wakati wa kurejea nyumbani kwani alikuwa ametenga siku tatu za kufahamiana ana kwa ana naye.
Lakini anasema alipata somo hapo kwamba kila wakati Mtu anapoamua kuanza mahusiano ya kimapenzi mtandaoni ni vizuri kumueleza rafiki au Mtu mmoja unayemfahamu kuhusu mkutano wako , ilimambo yakienda mrama umemjulisha angalao Mtu mmoja.
Na ndilo jambo lililomponza Kwani licha ya jamaa wa mtandao kutowasiliana naye alikuwa na swahibu wake ambaye aliishi kwake kwa hizo siku tatu .
Jeje anacheka anapokumbuka kuwa baadaye yule Mtu aliwasiliana naye na kudai kuwa ‘Mbwa wake alikuwa mgonjwa’ mama huyu akisema ya ulimwengu ni mengi , aliuliza maswali asipate majibu , licha ya hayo hakukata tamaa.
Jeje anasema kwamba 'app' nyingi ya mitandao ambayo Mtu analipa fedha hasa za kimahaba ndio zenye watu wenye muelekeo, waume kwa wanawake wanakuwa na malengo dhabiti na wala sio mchezo au utapeli haya ni kulingana na uzoefu wake binafsi.
Jaribio la pili kufaulu kisha ndoa
Jeje hakukata tamaa na mara nyingine alitosa ndowano yake ya kujinadi kwenye mtandao wa kijamii , wakati huu alianza urafiki na Mtu mmoja wa asili ya mzungu kwa karibia mwaka mmoja walichumbiana kwa umbali kupitia barua Pepe na mitandao. Ila anasema kwamba wakati mwengine waliwasiliana kwa kupiga simu za video ambapo walionana .
Wakati huu mama huyu alihisi kama kwamba kulikuwa na mwelekeo .
“Baada ya mwaka mmoja tuliamua kuonana hatimaye ana kwa ana , siku hio nakumbuka rafiki wangu alinichukua kutoka uwanja wa ndege , na mmoja kwa moja kunipeleleka hadi kwa kaka yake . Jambo hilo lilinipa tumaini Kwani alikuwa ananifahamisha kwa watu wake wa Karibu “anasema Jeje
Licha ya kuwa jamii yake ilikuwa na maoni kinzani kuhusu urafiki Wao hasa kwa kuwa mwanamke huyu ni mweusi na mwanamume ni mzungu , yeye alisimama kidete na kusema kwamba alikuwa ameaumua na chaguo lake ni hilo . Katika wakati huo jamaa alimchumbia na baada ya muda wa kufunga ndoa .Hatimaye Jeje alikuwa mke . Anasema kwamba alijawa na mtiririko wa hisia za furaha na pia dukuduku ya kuishi na mtu mwenye asili na desturi tofauti . Lakini aliamini kuwa ahadi za mahaba yao na Malengo yao yangewasaidia kuishi kwa kuelewana.

Chanzo cha picha, Alice Njeri
Changamoto
Jeje anasema kuwa mtihani wa kupata mume mzuri kwenye mtandao aliupita, ila Sasa kuishi na mtu mwenye rangi na kuzaliwa katika desturi na tamaduni tofauti ndio changamoto . Yeye anasema ilibidi kwanza asome kuhusu tofauti za chakula alichozoea na cha mwenza wake .
“Unajua watu wengi weupe hula mikate kwa kila mlo , Yaani sandwich, sisi tumezoea kula chakula asilia ambacho kimejaa sahani hadi kinamwagika.Sasa ilibidi mimi na mume wangu tuelimishane Juu ya hayo na mengine mengi” Jeje anasema.
Hivi Sasa Jeje mama wa watoto wawili , changamoto ya pili ni hio ya kuwa watoto Wao wanaasili mbili tofauti Kwa hio mama na Baba wamechukua majukumu ya kuhakikisha kuwa watoto Wao wanaelewa asili hizo mbili. kwa mfano Jeje anasema anawafunza wanae lugha yake ya asili kutoka Kenya , Kabila la Kikuyu .
Kwa upande mwengine wa baba au mume wake inakuwa rahisi kwani wako mazingira ya nyumbani kwao na watu wengi wa jamii yake wako huko , Kwa hio hilo limefanya utangamano Wao katika ngazi ya kijamii kuwa Mwepesi.
Jeje ni nani
Jeje alizaliwa nchini Kenya zaidi ya miaka 30 iliyopita , ni mama ambaye ameng’ang’ana sana kutafuta riziki nje ya nchi. Akiamini kuwa muhimu ni kupiga Moyo konde hakuna sehemu ambayo binadamu hawezi kufanikiwa, mradi ajitume.
Anasema kwamba amesafiri nchi za Dubai na Sudan kusini kutafuta maisha . Na hadi anapoishi Sasa Marekani anafahamu kwamba licha ya misukosuko mingi ya maisha ndoto zake zinatimia.