Mwalimu aliyepoteza kazi kwa kutuma picha zake Instagram

Chanzo cha picha, Getty Images
Chuo kikuu maarufu binafsi katika mji wa mashariki mwa India wa Kolkata (uliofahamika awali kama Calcutta) kimegubikwa na utata katika miezi ya hivi karibuni.
Profesa msaidizi wa zamani katika chuo kikuu cha Mt Xavier aliiambia BBC kuwa alilazimika kuacha kazi yake kwa kuwa alichapisha picha zake zilizoonesha akiwa amevaa nguo ya ndani aina ya bikini kwenye mtandao wa kijamii wa Instagram.
Mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 31, ambaye aliomba jina lake lisitajwe, aliwashutumu maafisa wa chuo hicho kikuu kwa " kumnyanyasa kingono " na anasema "alitishwa, kudhalilishwa na kuchunguzwa maadili."
Pia aliwasilisha malalamiko kwa polisi na kutuma taarifa ya kisheria kwa taasisi, ambayo ilijibu kwa kumshutumu kwa kuichafulia jina na kudai ilipwe rupia milioni 990 (takriban dola milioni $2.4) kama fidia.
Walinipeleka katika chumba cha upelelezi
Profesa msaidizi anasema kwamba alijiunga na kitivo tarehe 9 Agosti , 2021 kwa ajili ya kufundisha somo la Kiingereza kwa wanafunzi wanaosomea shahada.
Miezi miwili baadaye, aliitwa katika ofisi ya mkuu wa chuo kwa ajili ya mkutano.
Aliongozwa "hadi katika chumba cha upelelezi" ambako alihojiwa na kamati inayojumuisha Makamu mkuu wa chuo Felix Raj, katibu wa chuo Ashish Mitra na wanawake watano.
Alifahamishwa kuwa kulikuwa na malalamiko dhidi yake yaliyotolewa na baba wa mwanafunzi wa kiume anayesomea shahada.

Chanzo cha picha, Getty Images
"Mkuu wa Chuo alisema kwamba baba huyu alimpata mwanaye wa kiume akizitazama picha zangu kwenye Instagram ambapo nilikuwa nimevaa nguo ya ndani. Alisema picha zilikuwa zinaonesha utupu na akakiomba chuo kikuu kimuepushe mwanaye na uchafu wa aina hiyo."
Wajumbe wa bodi walizungusha kipande cha karatasi kilichokuwa na "picha tano- sita " na kumuomba athibitishe kwamba zilikuwa ni zake.