Mkutano Mkuu wa CCM wafikia tamati,

Chanzo cha picha, CCM
Mkutano Mkuu wa 10 wa Chama cha Mapinduzi CCM umemalizika leo katika mji mkuu wa Tanzania Dodoma ambapo rais wa nchi hiyo Samia Suluhu Hassan amepitishwa katika nafasi ya mwenyekiti kwa muda wa miaka mitano.
Sambamba na hilo, pia kumechaguliwa makamu mwenyekiti wa Bara na Zanzibar pamoja na wajumbe 40 wa Halmashauri Kuu kati ya 374 waliowania nafasi hizo.
Rais Samia amesema uchaguzi huu ni sehemu ya maandalizi kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.
“Ni wajibu wa kila mwanachama aliyeteuliwa na chama kugombea nafasi aliyoomba, kutambua kwamba lengo la uchaguzi uliokwisha kufanyika na utakaofanyika sio kutafuta ushindi wa mtu mmoja mmoja bali ni mkakati wa kujiimarisha na kujipanga kwa ajili ya kutafuta ushindi wa chama chetu kwa ajili ya chaguzi zijazo,” amesema rais Samia.
Wakati hayo yakijiri, upinzani nchini Tanzania wamekuwa wakilalamika kukosekana kwa fursa sawa za kunadi sera zao ikiwemo kufanya mikutano ya hadhara.
Maelfu ya wajumbe waliohudhuria Mkutano huo walijawa na hisia mchanganyiko huku baadhi yao wakihofia kuibuka kidedea katika uchaguzi uliofanyika.
Katika mkutano huo, pia kumeshuhudiwa utekelezaji wa mabadiliko ya katiba ikiwemo kutoa fursa kwa viongozi kuvaa kofia mbili katika uongozi wa juu.
”Baada ya hatua hii ya rais Samia kuchaguliwa kuongoza chama chake kwa miaka mitano, hivi sasa shauku kubwa iliopo miongoni mwa wananchi ni je, ataendelea na safu yake ile ile ya uongozi au ataamua kupangua pangua.”
Kwa upande wa wananchi, iwapo kutafanyika mabadiliko ya uongozi, matumaini yao ni kupata viongozi watakaoleta mabadiliko.
Mwajuma Selema ambae ni mwanachama wa CCM anasema iwapo rais atapangua safu ya uongozi wa Chama, basi angetamani kuona rais Samia akiweka viongozi wenye utashi wa kupambana na rushwa.
Nae John Bin John ambae ni mkazi wa Dodoma anasema, hana matumaini yoyote ya mabadiliko katika uchaguzi uliofanyika ndani ya chama tawala.
”Sina mategemeo yoyote kwa uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi, kwa sababu kinacholeta maana ya chaguzi ndani ya chama na wanaopanga safu ndani ya chama, ni kutafuta maisha bora kwa mtanzania, lakini kwa hatua tuliyonayo sasa hivi, ni kwamba wanapofanya chaguzi wanataka manufaa ya wao na familia zao, lakini sio kwa ajili ya watanzania,” amesema John.
Mkutano huu unafanyika wakati ambapo katika siku za hivi karibuni kumeshuhudiwa majibizano makali kati ya wana CCM kufuatia kauli ya aliyekuwa katibu mkuu wa chama hicho Dk Bashiru Ali iliyodaiwa kuikosoa serikali.
Joseph Butiku, kutoka Taasisi ya Mwalimu Nyerere anasema hakuna mpasuko wowote nda.
Hii ni hatua muhimu ya kujiimarisha kisiasa kwa chama tawala, lakini kwa upande wa upinzani, nyota inaonekana kuzidi kufifia.
Jawadu Mohammed ambae ni mchambuzi wa masuala ya kisiasa na uchumi anakiri kwa upinzani kutopewa fursa sawa lakini anasema bado wana nafasi ya kuweka mikakati, ikiwemo kufanya mikutano ya ndani na kuja na sera mpya.
”Kumekuwa na tatizo kwa vyama vya upinzani hapa Tanzania, ya kwamba, pamoja na mambo mazuri ambayo upinzani huonyesha, lakini upinzani wa Tanzania wamejielekeza zaidi kutumia madhaifu madogo na makosa ya CCM katika kujinadi kwa watanzania,” amesema Jawadu.
Mjadala unaoendelea hivi sasa ni iwapo ongezeko la idadi ya wajumbe kutoka 30 hadi 40 kutaongeza ufanisi ndani ya chama hicho au la, ni suala la muda.