Muitikio wa hedhi salama bado mdogo kwa Wanaume Tanzania

Upatikanaji wa pedi ni changamoto bado kwa wanafunzi wa sekondari nchini Tanzania
Maelezo ya picha, Upatikanaji wa pedi ni changamoto bado kwa wanafunzi wa sekondari nchini Tanzania

Mzunguko wa siku za hedhi kwa wanawake ni jambo ambalo huwa halizungumzwi hadharani katika jamii nyingi barani Afrika kutokana na imani za kidini na kitamaduni.

Vivyo hivyo ushiriki wa wanaume katika suala la hedhi kwa msichana nchini Tanzania lina pande mbili, baadhi wanaunga mkono na wengine wanapingana nayo na kuona kwamba ni suala la siri.

Licha ya kuepo kwa kwa kampeni na harakati nyingi hivi karibuni katika shule na vyombo vya habari bado muamko ni mdogo.

Kampeni hizi zinaibua hisia tofauti miongoni mwa jamii wapo ambao wanachukizwa wakiamini kuwa si jambo sahihi kuzungumzia suala la hedhi hadharani kwasababu tu ya tamaduni kitu ambacho kwa namna moja au nyingine husalia kama kizingiti katika harakati za kuleta uelewa juu ya hedhi hasa kwa vijana.

Wasichana wengi wa sekondari wanakumbana na changamoto kubwa ambayo inaadhiri masomo yao na kufifisha ndoto zao kutokana na kutokuwa katika mazingira mazuri yanayowafanya wawe na hedhi salama.

Maji safi na salama, matundu ya vyoo vya kutosha, walimu walezi wanaojali, bajeti ya kuwezesha shule kununua pedi kwa ajili ya wanafunzi vyote hivyo ni changamoto kwao.

Halima Mohamed kutoka Taasisi ya TAI- Tanzania inayotoa elimu ya hedhi kwa vijana ni muhamasishaji ambaye anahamasisha watu kuchangia pedi huzikusanya na wanazipeleka kwenye shule mbalimbali anasema zoezi hilo linachukua muda mrefu kwa sababu muitikio bado ni mdogo.

Wakati Doreen Temba yeye pia anashiriki katika kutoa pedi bure shuleni,anasema waliamua kufanya shughuli hiyo ili kueza kuwabakiza watoto wa kike shuleni maana huwa wanajisikia aibu kutokana na kukosa kitu cha kujistiri,zamani walikuwa wanatumia khanga,vitenge ambazo zilikuwa hazisaidii.

Kugawa pedi bure ndio suluhisho la changamoto za hedhi kwa wasichana
Maelezo ya picha, Kugawa pedi bure ndio suluhisho la changamoto za hedhi kwa wasichana

Leon ni meneja mradi wa JALI, mradi huu ulianzishwa maalum ili kuweza kutafuta suluhisho mbadala kwa wasichana wa shule za secondary, kuweza kujisitiri kwa kipindi kirefu pindi wawapo katika hedhi.