Gisèle Pelicot: Jinsi mwanamke aliyebakwa na 'wanaume wa aina zote' alivyogeuka kuwa shujaa

Tahadhari : Simulizi hii ina maelezo ya unyanyasaji wa kijinsia.
Kila asubuhi, foleni zilianza kupangwa kabla ya mapambazuko. Vikundi vya wanawake walisimama katika baridi ya msimu wa vuli kwenye barabara ya lami kando ya barabara yenye shughuli nyingi, nje ya mahakama ya Avignon.
Walikuja, siku baada ya siku. Wengine walileta maua. Wote walitaka kuwa mahali pa kumshangilia Gisèle Pelicot alipokuwa akitembea, na kupanda ngazi kupitia milango ya vioo vya jengo la mahakama. Wengine walithubutu kumsogelea.
Wachache walipiga kelele: "Tuko pamoja nawe, Gisèle," na "Uwe jasiri."
Wengi wao walibaki, wakitumaini kupata viti katika chumba cha mahakama kilichojaa watu wengi ambapo wangeweza kutazama kesi kwenye skrini ya televisheni. Walikuwa pale kushuhudia ujasiri wa bibi huyo , akiwa ameketi kimya mahakamani, huku akiwa amezungukwa na makumi ya wabakaji wake.
"Ninajiona kama yeye," alisema Isabelle Munier, 54. "Mmoja wa wanaume waliokuwa kwenye kesi licha ya kwamba mmoja alikuwa rafiki yangu. Inachukiza."
"Amekuwa kiongozi wa watetezi wa jinsia ya kike," alisema Sadjia Djimli, 20.
Lakini walikuja kwasababu nyingine pia.
Zaidi ya yote, ilionekana, walikuwa wakitafuta majibu. Wakati Ufaransa inatafakari matokeo ya kesi yake kubwa zaidi ya ubakaji, ambayo inamalizika wiki hii, ni wazi kuwa wanawake wengi wa Ufaransa - na sio tu wale walio katika mahakama ya Avignon - wanatafakari maswali mawili ya msingi.

Swali la kwanza kesi hii Inaweza kusema nini kuhusu wanaume wa Ufaransa - wengine wangesema wanaume wote - kwamba 50 kati yao, katika kitongoji kimoja kidogo cha mashambani, walikuwa tayari kukubali mwaliko wa kawaida wa kufanya mapenzi na mwanamke asiyejulikana akiwa amelala, amepoteza fahamu, kwenye chumba cha kulala?
Swali la pili linaibuka kutoka kwa la kwanza: je, kesi hii itafikia wapi katika kusaidia kukabiliana na janga la unyanyasaji wa kijinsia na ubakaji unaosababishwa na dawa za kulevya, na katika kutoa changamoto kwa chuki na ujinga kuhusu aibu na ridhaa?
Kwa ufupi, je, msimamo wa ujasiri wa Gisèle Pelicot na azimio lake - kama alivyosema, kufanya "mabadilishano ya aibu" kuanzia kwa muathirika hadi kwa mbakaji - itabadilisha chochote?
Nyuma ya nyuso za washtakiwa
Kesi ya muda mrefu huunda hisia zake na , katika wiki zilizopita, hali ya kushangaza ilijitokeza ndani ya mahakama ya Palais de Justice ya Avignon. Katikati ya kamera za runinga na misururu ya mawakili, kuonekana kwa watu kadhaa wanaodaiwa kubaka - nyuso ambazo hazikufichwa kila mara nyuma ya vinyago - hazikuchochea tena mshtuko uliokuwa nao mwanzoni.
Washtakiwa walitembea huku na kule wakipiga soga, wakitania, wakichukua kahawa kutoka kwenye mashine za kutengeneza kahawa au wakirudi kutoka kwa mkahawa kando ya barabara, na, katika mchakato huo, kwa namna fulani walisisitiza hoja ya msingi ya mikakati yao mbalimbali ya utetezi: kwamba hawa walikuwa watu wa kawaida tu. "[Hoja hiyo ni] jambo la kushtua zaidi kuhusu kesi hii.
Inasikitisha kuifikiria," anasema Elsa Labouret, ambaye anafanya kazi katika kundi la wanaharakati wa Ufaransa, Dare to be Feminist.
"Nadhani watu wengi walio na uhusiano wa muda mrefu na wanaume wanafikiria wapenzi wao kama mtu anayeaminika. Lakini sasa kuna hisia hii ya utambulisho wa [Gisèle Pelicot] kwa wanawake wengi. Kama ni 'sawa, inaweza kutokea kwangu' .
''Kwa hiyo, inawezekana mambo kama hayo yanafanyika kila mahali."
Taasisi ya Sera za Umma ya Ufaransa ilitoa takwimu za mwaka 2024 zinazoonyesha kwamba kwa wastani, 86% ya malalamiko ya unyanyasaji wa kijinsia na 94% ya ubakaji aidha hayakufunguliwa mashtaka au hayakufikishwa mahakamani, katika kipindi cha kati ya 2012 na 2021.
Bi Labouret anasema kuwa unyanyasaji wa kijinsia hutokea wakati wanaume fulani wanajua kwamba "wanaweza kuondokana nao. Na nadhani hiyo ni sababu kubwa ya ni kwanini unyanyasaji huu umeenea sana nchini Ufaransa."
'Si katili wala watu wa kawaida'
Katika kipindi chote cha kesi hiyo iliyodumu kwa miezi minne, kila mwisho wa mapumziko ya chumba cha mahakama, washtakiwa walikuwa wakikusanyika kabla ya kuwasogelea waandishi wa habari wengi wao wakiwa ni wanawake, pia wakisubiri kuingia ndani ya chumba hicho. Mle ndani, mmoja baada ya mwingine, wanaume hao walichukua zamu yao ya kushirikishana ushahidi wao.
Mtaalamu wa magonjwa ya akili aliyeteuliwa na mahakama Laurent Layet alitoa ushahidi kwamba washtakiwa hawakuwa "wanyama" wala "wanaume wa kawaida". Wengine walilia. Wachache walikiri. Lakini wengi walitoa visingizio vingi, huku wengi wakisema walikuwa "watu wenye uhuru" - kama Wafaransa walivyosema - wakitoa mawazo ya wanandoa, na kwamba hawakuwa na njia ya kujua kwamba Bi Pelicot hakukubali. Wengine walidai Dominique Pelicot alikuwa amewatisha.

Chanzo cha picha, Getty Images
Kuna mifumo michache sana iliyo wazi au sifa zinazoshirikiwa kati ya wanaume 51 walio kwenye kesi. Wanawakilisha wigo mpana katika jamii: robo tatu wana watoto. Nusu wameoa au wamo katika uhusiano. Zaidi ya robo yao walisema wamenyanyaswa au kubakwa wakiwa watoto.
Hakuna mgawanyiko unaotambulika kulingana na umri au kazi au tabaka la kijamii. Sifa mbili wanazoshiriki wote ni kwamba ni wanaume, na kwamba waliwasiliana kwenye jukwaa haramu la gumzo la mtandaoni liitwalo Coco, linalojulikana kwa huduma ya kubadilishana wapenzi kwa ajili ya ngono, na vilevile kuwavutia wafanyabiashara wa dawa za kulevya.
Kulingana na waendesha mashtaka wa Ufaransa, tovuti hiyo ambayo ilifungwa mapema mwaka huu, imetajwa katika ripoti zaidi ya 23,000 za uhalifu.
BBC imegundua kuwa 23 kati ya wale walioshtakiwa - au 45% - walikuwa na hatia za uhalifu hapo awali. Ingawa mamlaka hazikusanyi data sahihi, kulingana na baadhi ya makadirio ambayo ni takriban mara nne ya wastani wa kitaifa nchini Ufaransa.
"Hakuna utambulisho wa kawaida wa wanaume wanaofanya unyanyasaji wa kijinsia," alihitimisha Labouret.
Mtu mmoja ambaye amefuatilia kesi hiyo kwa karibu zaidi kuliko wengi ni Juliette Campion, mwandishi wa habari wa Ufaransa ambaye amekuwa mahakamani wakati wote wa kesi kuripoti kwa shirika la utangazaji la Ufaransa Info. "Nadhani kesi hii ingeweza kutokea katika nchi nyingine, bila shaka. Lakini nadhani inasema mengi kuhusu jinsi wanaume wanavyowaona wanawake nchini Ufaransa... Kuhusu dhana ya ridhaa," anasema.
"Wanaume wengi hawajui ridhaa ni nini hasa, kwa hivyo [kesi] inasema mengi kuhusu nchi yetu, kwa kusikitisha."
"Suala la Mr Everyman"
Kesi ya Pelicot hakika inasaidia kuuelewa mwelekeao wa mitazamo ya ubakaji kote Ufaransa.
Mnamo tarehe 21 Septemba, kundi la wanaume mashuhuri wa Ufaransa, wakiwemo waigizaji, waimbaji, wanamuziki na waandishi wa habari, waliandika barua ya umma ambayo ilichapishwa katika gazeti la Liberation, wakisema kwamba kesi ya Pelicot ilithibitisha kwamba unyanyasaji wa wanaume "sio suala la makatili".
"Ni suala la wanaume, la Mr Everyman[ kila mwanaume]," barua hiyo ilisema. "Wanaume wote, bila ubaguzi, wananufaika na mfumo unaowatawala wanawake."
Pia ilichora "ramani ya muongozo" kwa wanaume wanaotaka kupinga mfumo dume, kwa ushauri kama vile "tuache kufikiria kuna asili ya kiume ambayo inahalalisha tabia zetu".
Wataalamu wengine wanaamini kuwa maslahi makubwa ya umma katika kesi ya Pelicot yanaweza kuwa tayari kuzalisha faida.
"Kesi hii yote ni muhimu sana kwa kila mtu, kwa vizazi vyote, kwa wavulana wadogo, kwa wasichana wadogo, kwa watu wazima," anasema Karen Noblinski, wakili wa Paris aliyebobea katika kesi za unyanyasaji wa kingono.
"Imeongeza ufahamu kwa vijana. Ubakaji haufanyiki kila mara kwenye baa, kwenye klabu. Inaweza kutokea nyumbani kwetu."
Kampeni ya Hashtag ya NotAllMen [Sio wanaume wote]
Lakini ni wazi kuna kazi nyingi zaidi ya kufanywa. Nilienda kukutana na Louis Bonnet , ambaye ni meya wa kijiji cha nyumbani cha Pelicot, Mazan, mapema katika kesi. Ingawa hakuwa na shaka katika kulaani madai ya ubakaji, alisema kwa uwazi na mara mbili kwamba alihisi uzoefu wa Gisèle Pelicot ulikuwa umezidiwa, na akasema kwamba kwa vile alikuwa amepoteza fahamu, alikuwa ameteseka kidogo kuliko waathiriwa wengine wa ubakaji.
"Ndio, ninaipunguza, kwa sababu nadhani inaweza kuwa mbaya zaidi," alisema wakati huo.
"Wakati kuna watoto waliohusika, au wanawake kuuawa, basi hilo ni linakuwa jambo baya sana kwa sababu huwezi kurudi nyuma. Katika kesi hii, familia itabidi ijijenge yenyewe. Itakuwa ngumu, lakini hakuna aliyekufa."
Maoni ya Bonnet yalichochea hasira kote Ufaransa. Baadaye Meya alitoa taarifa, akiomba "msamaha wa dhati".

Chanzo cha picha, Reuters
Mtandaoni, mijadala mingi inayohusu kesi hiyo imelenga pendekezo lenye utata kwamba "wanaume wote" wanaweza kubaka. Hakuna ushahidi wa kuunga mkono dai kama hilo. Baadhi ya wanaume wamerudi nyuma dhidi ya hoja hiyo, wakitumia alama ya reli #SioWanaumeWote.
"Hatuwaombi wanawake wengine kubeba 'aibu' ya wanawake wenye tabia mbaya, kwanini kuwa mwanamume ifanye kubeba aibu hiyo");